Habari
BRELA KULETA MRADI WENYE SULUHU KWA WAKULIMA NA WAFUGAJI
Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), kwa kushirikiana na Shirika la Miliki Ubunifu Duniani (WIPO) na Taasisi washirika imefanya uzinduzi wa Mradi wa upatikanaji wa teknolojia rahisi itakayotumika kutengeneza chakula cha mifugo na mbolea kwa kutumia mabaki ya chakula na zao la Parachichi leo, Juni 01, 2026, Jijini Dar es Salaam.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mradi huo, Mkurugenzi wa Miliki Ubunifu kutoka BRELA Bi. Loy Mhando, alieleza kuwa, BRELA inajukumu la kulinda Miliki Ubunifu nchini na imekuwa ikifanya kazi kwa karibu na Shirikika la Miliki Ubunifu Duniani (WIPO). Kupitia ushirikiano wa kimkakati, BRELA iliwasilisha ombi la kutafuta teknolojia sahihi na madhubuti itakayosaidia kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini kutoka katika kanzidata ya WIPO ili ziweze kutumika kwa maendeleo katika jamii.
“BRELA ndio ofisi kiungo wa Miliki Ubunifu Tanzania Bara, na inafanya kazi kwa karibu na WIPO ambapo kutokana na ushirikiano huo tulifanya mawasiliano na tukaona umuhimu wa kwenda mbali zaidi ya kulinda Miliki Ubunifu kwa kuangalia ni namna gani tunatumia Miliki Ubunifu kwa maendeleo ya jamii, ndipo matokeo ya Mradi huu ambao unazinduliwa leo. Mradi huu unalenga kutafuta teknolojia rahisi itakayowezesha uzalishaji wa chakula cha mifugo na mbolea kwa kutumia mabaki ya vyakula” alisema Bi. Mhando.
Bi. Mhando alibainisha kuwa Mradi huo utaanza kutekelezwa kwa majaribio katika mikoa ya Nyanda za Juu Kusini ikihusisha mikoa ya Mbeya, Iringa, na Njombe kwa lengo la kuwanufaisha moja kwa moja wakulima na wafugaji nchini.
Aliendelea kusema kuwa mradi huu utatafuta na kuleta teknolojia ambayo itatumia mabaki ya vyakula kuzalisha bidhaa nyingine. Hatua hii haitainua tu jamii kiuchumi, bali pia itapunguza kwa kiasi kikubwa mzigo wa Serikali na wafanyabiashara kuagiza vyakula vya mifugo kutoka nje ya nchi.
Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Uratibu wa Mradi kutoka WIPO Bw. Purevdorj Vaanchig, alifafanua kuwa lengo la Mradi huo ni kujenga uelewa mpana na kuwajengea uwezo watafiti wa Vyuo Vikuu Nchini. Alisisitiza kuwa hatua hiyo itawawezesha wadau hao wa kitaaluma kuelewa matumizi ya Teknolojia sahihi ili kuleta matokeo chanya na mabadiliko ya kimaendeleo katika jamii.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Bw. Amos Nungu, alieleza manufaa ya mradi huo kwa vijana wa Kitanzania, akibainisha kuwa kukamilika kwake kutasaidia vijana kupata haki za Miliki Ubunifu, kuwa wabunifu zaidi, na kutengeneza sampuli-kifani zitakazokuwa rahisi kuingia na kushindana sokoni. Aliongeza kuwa, baada ya Mradi huo kufanikiwa katika maeneo hayo ya awali, utasambazwa nchi nzima ili kuleta maendeleo jumuishi.
Akigusia upande wa utafiti na taaluma, Mkurugenzi wa Utafiti na Ubunifu kutoka NM-AIST, Prof. Thomas Kivevele, alisisitiza kuwa lengo kubwa la Mradi ni kukuza uwezo wa ndani wa Watanzania. Alieleza kuwa kupitia wataalamu waliopo katika Taasisi ya NM-AIST, wataweza kugeuza maarifa ya kitafiti kuwa suluhisho la vitendo kwa jamii za vijijini, jambo litakalowasaidia wananchi kuelewa teknolojia hizo na kubuni nyingine nyingi zaidi kwa ajili ya kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na wa Taifakwa ujumla.
Mwakilishi wa wanufaika wa Mradi huo, Bi. Anna Upendo Gombela ambaye ni Mkulima na Mfugaji kutoka Mkoani Njombe, alionesha matumaini makubwa akisema, endapo wataalamu wetu watafanikiwa kutengeneza mashine hizi za ubunifu zitakazosaidia kutengeneza vyakula vya mifugo na mbolea kutokana na mabaki ya chakula, zitatubadilishia maisha. Zitatusaidia kupata chakula cha mifugo kwa wakati na kwa urahisi, kuongeza thamani ya kazi yetu, na kupunguza gharama kubwa za ufugaji zinazotokana na uhaba wa chakula.
Uzinduzi huo umehusisha pia taasisi mbalimbali washirika zikiwemo, Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST).
Uzinduzi wa Mradi huu unaongozwa na kaulimbiu isemayo: "Kukuza kilimo mzunguko kupitia ubunifu: Kugeuza utafiti kuwa teknolojia nafuu na endelevu za chakula cha mifugo." Kufuatia uzinduzi huu, mafunzo ya siku tano yatatolewa kuanzia leo tarehe 01 hadi Juni 05, 2026. Mafunzo hayo yatahusisha pia mijadala ya kina kati ya wajumbe wa kamati ya usimamizi wa mradi, timu ya utekelezaji, pamoja na wataalamu wa kitaifa na kimataifa ili kuweka sawa hatua muhimu za utekelezaji na matokeo
