Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni

Tunaipa Uhai wa Kisheria Biashara yako

Habari

BRELA KUTATUA CHANGAMOTO ZA WAFANYABIASHARA TANGA


BRELA KUTATUA CHANGAMOTO ZA WAFANYABIASHARA TANGA

Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), imewataka wafanyabiashara nchini kutumia fursa ya Maonesho ya 11 ya Biashara na Utalii ya Tanga -2024 kutatua changamoto mbalimbali zinazojitokeza zikiwemo urasimishaji wa biashara pamoja na uhuhishaji wa taarifa za Kampuni.

Afisa Sheria wa BRELA Bw. Lupakyiso Mwambinga, ameyasema hayo leo tarehe 30 Mei, 2024 katika banda la BRELA lililopo katika viwanja vya Usagala mkoani Tanga.

“Maonesho haya ni muhimu, ukizingatia kwamba hivi sasa masuala ya uboreshaji wa mazingira ya biashara na uwekezaji ikiwemo usajili wa majina ya biashara na Kampuni, usajili wa Alama za Biashara na Huduma pamoja utoaji wa Leseni za Biashara na Viwanda yanafanyika kwa njia ya mtandao kupitia Mifumo ya Kielektroniki au mifumo ya TEHAMA hivyo ni vyema wadau wakajitokeza kwa wingi ili kuhakikisha wanapata huduma za BRELA ,” amesema Bw. Mwambinga.

Ameeleza kuwa , maonesho haya yatakuwa chachu kwa wafanyabiashara, ambao hawajasajili biashara zao na kuhuisha taarifa za Kampuni ambapo wataweza kufanya mabadiliko mbalimbali ya sajili zinazotolewa na BRELA pia ametumia fursa hiyo kuwakaribisha wadau kufika katika banda la BRELA kwani huduma zote zinatolewa papo kwa papo.

Ameongeza kuwa ushiriki wa BRELA katika maonesho haya kwa wafanyabiashara ni nyenzo ya kupunguza kero, changamoto mbalimbali zinatokana na kutokuwa na uelewa wa kutosha wa mifumo ya usajili hivyo ametoa rai kwa wadau wa biashara nchini kujitokeza kwa wingi kupata huduma hiyo.

Maonesho haya ya 11 ya Biashara na Utalii (Tanga Trade Fair -2024) yaliyoandaliwa na Chemba ya Biashara, Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa yanatarajia kufunguliwa rasmi tarehe 3 Juni, 2024 katika viwanja vya Usagala mkoa wa Tanga.